Pages

Friday, September 27, 2019

WAISLAMU NA BIDHAA ZA KIFEDHA-SEHEMU YA PILI.


Karibu! Katika sehemu ya kwanza ya makala haya tulionyesha kuwa mambo matatu-Riba, Gharar na Maisir-kuwa ni mambo yenye kutiya doa mfumo wa kifedha wa ulimwengu. Tukatoa mfano wa njia mbadala ili kuepukana na madoa hayo katika sekta ya benki. Leo tutaingalia sekta ya bima.

Sekta ya Bima. Bima kwa ufupi ni utaratibu ambao unaomuwezesha mtu au biashara kujikinga na athari mbaya za matukio ya hatari (insurable risk) kwa kukuwezesha kifedha kurudi katika hali yako ya awali. Kwa mfano, hatari za kuunguliwa nyumba yako inaweza kupunguzwa kwa kupitiya bima ya moto ambapo kampuni ya bima hukulipa kiwango cha fedha ambacho utaweza kujenga nyumba yako kama ile ya mwanzo na kuendeleya na maisha. Hatari ya kuumwa na magonjwa na ikawa hauna hela ya kulipiya matibabu pia bima ya afya inakuwezesha kupata fedha ambazo hulipwa katika kituo cha afya ili upate huduma ya matibabu. Hizo ni baadhi ya hatari, hatahivyo hatari zipo aina nyingi, baadhi yake kuhatiwa bima na nyingine hazina bima kama vile vita (war), fujo (riots) n.k.

Uislamu unatambuwa haja ya kuwa na utaratibu ambao unawawezesha wananchi kujikwamuwa au kusaidiana wanapopatwa na hatari mbalimbali katika maisha yao na shughuli zao. Hivyo Uislam hauna pingamizi na dhana ya bima iwapo utaratibu wa shughuli za bima hizo utaachana na madoa yale matatu-RIBA, GHARAR, MAISIR na Uwekezaji ktk sekta ambazo ni kinyume na maadili. Kwa bahati mbaya, katika nchi zetu na duniani kote, bima zote zinamadoa hayo isipokuwa zile zinazoitwa za TAKAFUL (Bima inayofuta kanuni na maadili ya kiislamu). Bima aina hii (TAKAFUL), mkataba wake sio wa mauzo ya kuhamisha hatari ( not a sales contract to transfer risk) kutoka kwa mnunuzi wa bima kwenda kwa muuzaji bali mkataba wake ni wa kujumuika pamoja kusaidiana na kushirikiana katika kuondoa athari za hatari ( contract of partnership / co-operation in sharing the risk). Wanaojiunga na utaratibu wa takaful, wanakubaliana kushirikiana kumsaidiya mwenzao pale anapopatwa na janga au hatari fulani kwa kuchangia fedha kiwango maalum (contribution) na kuwekwa katika mfuko (pooled fund) ambazo zitawekezwa katika vitega uchumi halali (visivyokuwa na riba) ili michango hiyo na mapato yake yaongeze uwezo wa mfuko kukabiliana na athari za majanga yanayoweza kuwakumba wachangiaji wake na kuwalipa mara kwa mara (claims). Mfuko huo wa fedha utasimamiwa na kampuni (Takaful operator) ambayo itahakikisha kila mchangiaji anapewa kiwango stahili cha kuchangia (underwriting) na pia kuwekeza (investing) kwa niaba ya wachangiaji ambao ndio wamiliki wa mfuko huo. Msimamizi (Takaful operator) hulipwa kwa mujibu wa makubaliano maalumu. Kwa kupitiya utaratibu huu, doa la riba, gharar na maisir huwa limetatuliwa!

Inafahamika nchini Tanzania na sehemu nyinginezo kuwa baadhi ya wananchi hususani waislamu kamwe hawaridhii kushiriki katika BIMA hizi za kawaida isipokuwa kwa sababu ya KULAZIMISHWA tu na Sheria ambazo hazizingatii tamaduni na maadili yao. Kwa maneno mengine, wananchi hawa wanavumiliya tu sheria hizo ambazo zinawafanya wafanye kitendo haramu kwa mujibu wa dini yao. Ni wazi kuwa utaratibu wa kulazimisha watu kwa kuweka Sheria nje ya tamaduni za watu. Kadhalika Sheria hizo zinaenda kinyume na misingi ya somo la Legal anthropology ambalo mtaalamu wa sheria Profesa Palamagamba Kabudi amelifundisha na kuwahimiza wabunge na hususani wanasheria kulizingatiya wamapotunga sheria! Ni kwa kuzingatiya misingi ya somo hilo, kwa mfano nchi nyingi ikiwemo Tanzania katika Sheria yake ya ndoa inatambuwa matakwa ya dini mbalimbali katika suala la ndoa na hivyo Sheria inatambuwa ndoa ya mila, ndoa ya kiislamu na ndoa ya kiserikali. Kwa bahati mbaya, sera na sheria zinazohusu uchumi wa fedha (financial economy) hazijazingatiya tamaduni na maadili ya watu wake na hivyo watu wote kuwekwa katika mfumo mmoja tu wa kiserikali (government way and no other way!). Haya ni mapungufu makubwa na wahusika wanapaswa kuyatazama kwa kushirikiana na wahusika ili kuwa na sera na sheria jumuishi (inclusive financial policies and legislation).

Matokeo ya kukosekana TAKAFUL ni kuwa wananchi huathirika na nchi huathirika mno. Wananchi huathirika na matokeo ya majanga mbalimbali ambayo kimsingi yangeweza kuwa na BIMA ya TAKAFUL lakini kwa kuwa bima zilizopo ni HARAMU wanashindwa kujiunga nazo. Hivyo juhudi ya miaka ya mwananchi kujenga nyumba yake au kulima chamba lake n.k, inaweza kupoteya kwa janga moja tu la moto na kumpelekeya kuwa masikini omba omba mtaani. Au ugonjwa unaotibika unapelekeya matatizo makubwa kiafya pale familiya inaposhindwa kumudu gharama wakati BIMA ya TAKAFUL ingemuwezesha kumudu gharama za matibabu na kuokowa maisha yake. Wananchi wanavumiliya lakini ni njia njema ni wananchi waishi kwa kuvumiliya au kufurahiya?

Serikali piya huathirika mno. Serikali inakosa uwezo wa kukusanya akiba (saving mobilization) ipasavyo kuwa kupitiya taasisi za BIMA kwa ajili ya uwekezaji katika miradi ya maendeleo nchini kwa kuwa wananchi hawajiungi na bima hizo zanazokinzana na utamaduni / imani yao. Serikali inakosa mapato ya kodi kutoka katika faida ya makampuni ambayo yapo tayari kuendesha shughuli za bima kwa njia ya TAKAFUL na pia kukosa kodi ya mshahara (PAYE) ambayo ingelipwa na wafanyakazi wa makampuni hayo. Vile vile mzigo mkubwa kwa serikali katika kutowa huduma mbalimbali kama ya afya kwa kuwa wananchi hawamudu kuchangiya gharama zake. Vile vile, serikali kukosa uwekezaji katika sekta ya BIMA kwa kuwa sekta hiyo inatambuwa utaratibu mmoja tu na haitambui TAKAFUL. Mbaya zaidi, huduma za bima hazileti manufaa yanayotarajiwa kwa kuwa wananchi wahazipokei huduma hizo zenye kukinzana na tamaduni / imani zao.

Kwa kutambuwa hasara hizo, nchi mbalimbali duniani kama vile Uingereza, Malaysia, Indonesia, Afrika Kusini, Nijeria, Kenya, Misri, Sudani n.k wameruhusu utaratibu wa TAKAFUL katika nchi zao. Huduma hizo zinawanufaisha wananchi wote bila kubaguwa imani zao. Nchini Tanzania, wananchi walishaeleza haja yao ya kutaka huduma za TAKAFUL katika tafiti iliyofanywa na TIRA mwaka 2012. Tafiti hiyo ilianza kufanyiwa kazi kwa kutengenezwa kanuni (regulations) ambazo zitaiongoza TIRA katika utoaji wa leseni, usimamizi n.k. Wadau mbalimbali walishiriki katika kuzitengeneza na kuzipitisha. Lakini miaka zaidi ya minne, kanuni hizo hazitangazwa rasmi, Kulikoni?

Kwa kutambuwa ucheleweshaji wa jambo hili, Waziri wa Fedha Mh. Mpango katika hotuba yake kwa wadau iliyofanyika mkoa wa Tanga tarehe 27 Oktoba 2018 aliahidi kuwa mambo matatu wizara yake itayaingilia (ministerial intervention) na kuyatatuwa kwa haraka; la kwanza suala la kuwa na sera mpya ya shughuli za BIMA (National Insurance Policy), kanuni (regulation) za uendeshaji huduma mseto wa benki na bima (bancassurance) na kanuni za shughuli za Takaful. Mwaka mmoja ukiwa unakaribiya kitimiya tangu ahadi hiyo itolewe, bado kanuni za Takaful hazijatangazwa ilhali kuna makampuni kadhaa yasemekana yameshaomba kutowa huduma hizo katika mamlaka ya bima nchini (TIRA) lakini bado hayajaruhusiwa!

Wakati nchi na wananchi wanaathirika kutokana na kwa mapokezi hafifu ya huduma za bima (low insurance penetration rate), tunaiomba serikali yetu sikivu ilifuatilie suala hili na kumkumbusha Waziri wa Fedha kulimaliza suala hili ambalo ni kero kwa wadau na wananchi. Naamini TAKAFUL ikiruhusiwa na kuwekewa mazingira mazuri itaongeza kiwango cha wanaotumia huduma hizo mara dufu, kuwanufaisha wananchi na nchi nzima.

Kwa maelezo ya kina kuhusu TAKAFUL, soma;

https://www.findevgateway.org/sites/default/files/mfg-en-paper-takaful-and-poverty-alleviation-2004.pdf










Sunday, September 22, 2019

WAISLAMU NA BIDHAA ZA KIFEDHA-SEHEMU YA KWANZA.



Uislam ni mfumo kamili wa maisha ya mwanadamu. Mfumo huu kwa miaka zaidi ya 1441 umekuwa ikifuatwa na waislam duniani kote. Katika mfumo wa Uislamu, suala la fedha limefunzwa ipasavyo kiasi ambacho muislam hahitaji kujifunza nafasi, umuhimu na namna ya kutafuta au kuitumiya fedha kutoka kwa wasiokuwa waislam. Uislam katika fiqh yake una mlango mpana wa Fiqh Muamalat ambao ndani yake kuna mlango wa Fiqh al Masrafi Al Islam (Fiqh ya mambo ya fedha ya Kiislam).

Waislam wanaongozwa na misingi imara ya dini yao inayowataka waepukane na riba, gharar (udanganyifu, hatari isiyokuwa na ulazima), na maisir (bahati nasibu-upande mmoja upate na mwingine ukose) katika miamala ya biashara na fedha. Mambo matatu hayo yamekuwa ni doa kubwa au shimo la moto katika huduma za kifedha zilizozagaa ulimwenguni hivi leo. Na mambo hayo pamoja na kudorora kwa maadili mema, yamesababishiya ulimwengu kila baada ya miaka kumi au zaidi, kudorora kwa mfumo wa fedha na uchumi (financial crisis) au kuingiya katika shimo hilo la moto. Hivyo bidhaa nyingi za kibenki, bima, na masoko ya mitaji kwa kuwa na madoa hayo-yaani riba, gharar na maisir-muislamu hulazimika kuepuka bidhaa hizo kama ukoma au zaidi. Kutofanya hivyo ni kuchuma madhambi makubwa! Muislamu halisi anakumbuka kuwa kujihusisha na riba ni kutangaza vita na Muumba wake. Muislam halisi hatothubutu.

Waislam hao wanapojitenga na bidhaa hizo za kifedha, wao wanaathirika duniani kwa kiasi fulani lakini nchi husika piya inaathirika. Tutatowa mifano michache.

1. Huduma za kibenki. Benki nyingi huduma zake kwa kiasi kikubwa isipokuwa huduma chache tu zimezungukwa na riba ya kutisha. Huduma ya kufungua akaunti ya akiba, ukiweka pesa zako ili ziwe salama, benki hizo zinafanya mkataba na wewe wa kukupa riba ya kiasi fulani. Ukifungua akaunti ya hundi, bank hizo zinatumiya pesa hizo na za akiba kukopesha wengine na kuwatoza riba. Hivyo, inakuwa ni kupokeya riba au/na kuisaidiya bank kwa kupitiya hela zako kukopesha wengine kwa mikopo ya riba. Muislam katu hawezi kuhatarisha akhera yake kwa maslahi ya ulimwengu tu kwa kuziwezesha bank hizo kuendeleza uovu wa riba!

Je vipi muislam anaathirika? Muislam anaathirika kwa njia tatu, moja kukosa mahala salama pa kuweka fedha zake. Pili, anakosa mahala pa kuwekeza pesa zake ili kuzilinda fedha hizo dhidi ya mfumuko wa bei unaoshusha thamani ya pesa. Tatu, kukosa mahala pa kupatiya mtaji au rasimali (financing) ambayo itamuwezesha kukidhi mahitaji yake binafsi au ya biashara zake. Sidhani kama kuna serikali ambayo ingependa kuwawacha sehemu ya wananchi wake wapate shida hizo wakati ipo njia nzuri ya kuwasaidiya!

Je vipi nchi inaathirika? Nchi inaathirika mno. Kwanza, inakosa uwezo wa kukusanya akiba (weak saving mobilization) ambazo zinaweza kuwekezwa katika vitega uchumi mbalimbali. Tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa ukosefu wa akiba huchangiya nchi kuwa na maendeleo madogo. Kwa mfano ikiwa kunatakiwa uwekezaji mkubwa kwa ajili ya maendeleo ya nchi, mfumo wa kibenki unakuwa hauna hela za uwekezaji katika miradi hiyo. Matokeo yake, nchi inalazimika kukopa nje na kwa masharti ya ajabu ajabu ambayo haitonufaisha nchi ipasavyo. Vilevile wananchi wanakosa mitaji kwa gharama nafuu kwa sababu pesa nyingi zinakuwa nje ya mzunguko wa mabenki. Pili, sera za kifedha (monetary policy) zinashindwa kuwa na athari nzuri katika kuimarisha uchumi wa nchi kwa kuwa mzunguko mkubwa wa fedha upo nje ya taasisi za fedha. Tatu na mbaya zaidi ni kushindwa kuondowa umasikini kwa kupitiya mikopo. Waislam katu hawatachukuwa mikopo ya riba hata ikiwa riba hiyo ni 1%. Sasa mikakati ya kupambana na Umasikini inakuwa ni kwa maeneo ya wasiokuwa waislam lakini maeneo ya Zanzibar, Dar, Tanga, Lindi, Mtwara, Bagamoyo, Mwanza, Songea, Morogoro, Pwani, n.k utakuta hawachukuwi mikopo ya riba na hivyo harakati za kuondowa umasikini zinakuwa ngumu.

Tafiti kadhaa zinaonesha kuwa huduma za fedha zisizozingatiya imani na tamaduni za watu wake, hususiwa na watu hao. Kwa kuliona hili, nchi kadhaa ulimwenguni hata zenye waislam wachache, wameruhusu mfumo wa kibenki wa Kiislamu ambao hautozi au kupokeya riba na badala yake unasimama katika misingi ya kufanya biashara, uwekezaji na ushirikiano kwa kupitiya mikataba ambayo inakidhi kanuni na sheria za kifedha za kiislamu. Matunda mazuri ya mfumo wa kibenki wa Kiislamu unawavutiya hata wasiokuwa waislam kwa kuwa pamoja na kutotoza riba, unazingatia maadili mema katika kuchaguwa maeneo ya kuwekeza. Bank hizi zimejipambanuwa katika kujiepusha na uwekezaji katika biashara za ulevi, uasherati, kamari, silaha, utakatishaji fedha haramu, uzalishaji wa sigara na uharibifu wa mazingira pamoja na mambo mengine. Kwa kupiya huduma hizi na iwapo serikali husika itaweka mazingira rafiki, wananchi wengi watanufaika na nchi pia itanufaika sana. Kwa mfano nchi kama Uingereza, leo ni kitovu cha huduma za fedha za Kiislam! Wanajali maslahi ya kiuchumi kwa nchi yao na wananchi wao. Nchi hiyo imeweza kuvutiya wawekezaji na mitaji mikubwa kutoka nchi mbalimbali kuwekeza Uingereza japokuwa waislam ni sehemu ndogo. Katika afrika yetu, nchi kama Afrika kusini, Kenya, Nigeria zenye uchumi mkubwa zimejizatiti katika kuweka mazingira mazuri. Nchi na wananchi wote bila kujali dini zao wananufaika na huduma hizo.

Nchini Tanzania, Kenya na Uganda, tunazishukuru serikali kuruhusu uwepo wa benki ya Kiislam na huduma za kifedha za Kiislamu ambazo zimekuwa zikifanya vizuri japokuwa kwa kasi ndogo kutokana na changamoto mbalimbali. Ni wakati muwafaka kwa serikali kuwa na utaratibu mzuri na uliokuwa wazi na sheria zilizowazi (Legal, supervisory and regulatory framework), elimu ya bishara yenye kuwajuza wananchi kuhusu mabenki haya n.k. Hatuwa hizi na nyinginezo, zenye kutambuwa mfumo huu zitavutiya wawekezaji, kuongeza kukuza akiba (mobilize national savings through financial inclusion), kuzipa nguvu sera za kifedha katika kuimarisha uchumi na hivyo uchumi wa nchi na wananchi wetu.

Kwa kumaliziya nukta hii, nitowe wito kwa waislamu na wananchi wa imani zote kuweka fedha zao katika benki zenye huduma za kifedha za Kiislam. Na kwa Waislam hususani sehemu ambazo huduma hizo zinapatikana duniani, hawana sababu ya kuweka hela zao majumbani au katika taasisi nyingine au kuendeleya na miamala ya kibenki yenye kujihusisha na riba!

Itaendeleya...

Kwa maarifa zaidi, soma:
Ijuwe ubaya na hatari ya Riba, Gharar na Maisir kwa kusoma hapa:https://mpra.ub.uni-muenchen.de/67711/1/MPRA_paper_67711.pdf
Ijuwe Gharar kwa kusoma hapa : https://islamicmarkets.com/education/gharar.