Pages

Monday, July 20, 2020

HATARI YA MOTO NA HAJA YA BIMA YA KIISLAMU (TAKAFUL)



Mwaka wa 2019 na mwanzoni mwa mwaka huu, nchini Australia walipatwa na janga kubwa la moto katika misitu (bushfires) na mpaka katika makazi ya watu. Zaidi ya ekari 46 milioni ziliteketeya kwa moto, nyumba zaidi ya 3500 ziliunguwa na watu 34 walipoteza maisha.

Kwa masikitiko makubwa, mwezi huu baadhi ya shule za Kiislam kama vile Ilala Islamic, Mtambani, Kinondoni na kituo cha mayatima zilikumbwa na maafa ya kuunguwa kwa moto. Kwanza niwape pole wafiwa wa janga hili na waathirika wote wa moto huu na mingine iliyopita. Ni jambo la kusikitisha uhai na mali inapopoteya kwa mkasa wa moto au kwa janga lolote jingine. Kwa kuwa yameshatokeya, hatuna budi kuwa na subira na tunamuomba Mola atuepushe yasiendelee kutokeya maafa haya.

Binafsi nimekumbana na mtihani wa moto mara mbili katika maisha yangu. Mara ya kwanza, nikiwa shule ya msingi, nyumba yetu ilipatwa na mkasa wa kuunguwa na sehemu ya chumba kimoja iliathirika sana kisha moto huo ulizimwa kwa taufiki ya Allah kupitiya msaada ya majirani wema. Nakumbuka zahma na taharuki zake siku hiyo hazikuwa za kawaida. Mara ya pili, nikiwa chuo kikuu cha Kiislamu nchini Uganda, bweni letu lote lilichomeka kwa moto. Sikuweza kuokoa chochote zaidi ya nguo nilizokuwa nazo siku hiyo na ilikuwa karibu na muda wa mitihani ya kumaliza muhula. Ni mtihani mzito, uliotulazimu tulale msikitini kwa muda, tuazimwe nguo za kuvaa, kupewa nasaha (counselling) na mengi ya kueleza lakini hapa sio sehemu yake. Makala haya yatajaribu kusisitiza juu ya hatari ya janga la moto katika maisha yetu, athari yake kiuchumi na hatuwa za kuchukuwa ili kujihadhari na athari hizo.

Hatari na maafa ya Moto.

Maafa ya moto huenda yameanzia pale moto uliposhushwa na kutumika na binadamu ulimwenguni. Moto umetajwa katika vitabu vitukufu kama adhabu waliondaliwa waovu katika maisha ya Akhera kwa kuasi kwao maelekezo ya Mola wao. Ikiwa moto ni adhabu akhera kwa waovu, basi hili ni afa na janga kubwa na baya mno linaloweza kumpata binadamu duniani au akhera.

Siku moja wakati wa Mtume Muhammad s.a.w nyumba iliunguwa na kuunguza wakazi wake katika mji wa Madina. Mtume s.a.w akasema " Moto huu kwa hakika ni adui yenu. Mnapoenda kulala, hakikisheni mnazima sehemu zenye moto." (Sahih Bukhari). Katika hadithi nyingine kasema " Msiuwache moto unawaka katika nyumba zenu." Katika Qur'an, Allah s.w.t ametuagiza " Enyi Mlioamini, jiepusheni nyinyi na familia zenu kutokana na Moto." (66:6).

Vyanzo vya maafa ya kuunguliwa na moto ni anuai. Inaweza sababu ikawa ni hitilafu ya umeme (electrical), matumizi yasiyo sahihi ya majiko ya kuni, mkaa au gas (Cooking), sigara ambayo haikuzimwa, mishumaa na vifaa vya kutiya joto hasa katika maeneo ye baridi (heaters)na kadhalika. Kadhalika moto unaweza kusababishwa na watu wanaotaka kuhujumu wengine. Kimsingi, moto unapoleta maafa ni lazima vyombo vya uzimaji moto vifanye uchunguzi wa kina juu ya sababu yake na iwafahamishe wahusika sababu hizo. Katika nchi zilizoendeleya, matukio yote ya moto hurekeodiwa na sababu zake ili taarifa hizo ziwafae wananachi katika kuchukuwa tahadhari zaidi.

Athari za Kiuchumi.

Kuna nchi chache ambazo huweka taarifa ya gharama ya moto katika nchi zao kiuchumi. Nchini Uingereza na Wales, taarifa yao ya mwaka 2003 (Economic cost of fire report) imekisia kuwa gharama ya moto katika nchi hizo ni paundi 7.7 bilioni (sawa na Tzs 22 trilioni).

Katika moto uliotokeya Australia mwanzoni mwa mwaka huu, Wataalamu wa masuala ya bima walikisiya kuwa baina ya Nov 2019 mpaka kati ya Feb, 2020 moto huo ulisababaisha hasara inayokaribiya bilioni za marekani 1.3 kutokana na madai yaliyowasilishwa(insured claims) kwa makampuni ya bima. Mwaka 2015 katika nchi ya Indonesia, moto katika misitu yake na mazao yake yaliigharimu nchi hiyo dola za marekani bilioni 16.

Kiwanda kinapopata moto, wafanyakazi wenye ujuzi wanaweza kupoteza maisha yao, mashine na zama muhimu kuharibika, ajira kupoteya, uzalishaji kupunguwa n.k ni athari kubwa japokuwa sio rahisi kutathmini athari yake kifedha katika uchumi. Nyumba ya mtu inapatwa na janga hili, niwazi kuwa inamuathiri mtu kiuchumi kwa kukosa makazi yake salama na uwezekano wa kutumiya nyumba yake kama dhamana ya mikopo benki. Mbaya zaidi inamweka katika gharama ya kukodisha nyumba kila mwezi na kulipiya pesa kadhaa. Mifano hii michache itutosheleze kutambuwa kuwa moto iwe wa nyumbani au shuleni au kiwandani au ofisini unaathari kubwa kwa watu na mali zao na uchumi kwa ujumla.

Tathmini za awali za shule ya Ilala Islamic, Mvumoni na Kinondoni Muslim zinaonesha karibu nusu bilioni au zaidi zitahitajika ili kurekebisha hasara iliyojitokeza ya mali zilizopoteya lakini uhai hauwezi kurudi tena. Ikiwa taasisi hizo zinamkopo benki, wanaweza kuathirika katika kulipa mikopo na kusababaisha benki kuwa na mikopo mibaya (non-performing loans)


Hatuwa za kuchukuwa.

Kimsingi kuna hatuwa tatu za kukabiliana na tishio la moto katika nyumba au ofisi au kiwandani. Ya kwanza, ni kuchukuwa tahadhari ya kuepuka kuwa na matumizi ya moto kabisa katika nyumba au ofisi. Kusiwe na umeme, kusiwashwe kandili au mshumaa au matumizi ya kitu chochote cha moto, hii inaitwa ni ni kuepuka vyanzo vya hatari ya moto kabisa (risk avoidance). Hii ni njia ngumu kabisa kutekelezeka katika

Njia ya pili, ni kuendeleya na matumizi ya vitu vya moto na huku kuweka mitambo mbalimbali ya kugunduwa moto ukiwaka (fire sensors and alarms), njia za kuzimia maji za uhakika (fire water pipes), kamati za kuangalia na kutathmini majanga (crisis au disasters committees) ambazo zinaweza kuchukuwa hatuwa ya haraka janga linapotokeya n.k. Njia hii inalenga kupunguza athari ya uharibifu wa moto (risk reduction measure). Bado moto unaweza kutokeya na kuleta athari kiuchumi.

Njia ya tatu, ni kuhamisha athari ya kiuchumi ya janga la moto kwa kukata bima (Insurance -risk transfer). Kwa kupitiya bima ya moto, linapotokeya janga la moto katika nyumba au kiwandani au ofisini, kampuni ya bima itakuja kulipa gharama ya hasara iliyotokana na moto huo. Hivyo, bima inapunguza au kuondosha mzigo wa gharama ambazo zingehitajika kurekebisha nyumba au ofisi au kiwanda ili mwenyewe asikose makazi au asipatwe na gharama za kuijenga ofisi au nyumba kutoka mfukoni mwake. Lakini maisha ya watu hayawezi kurejeshwa kwa bima yoyote ile.

Kwa bahati mbaya na masikitiko makubwa, bima ya moto na zote zilizopo nchini ni HARAMU kwa waislamu kwa kuwa zinakwenda kinyume na sheria za mikataba ya biashara ya Kiislamu. Mikataba wa bima zilizopo unahusisha riba na kukosa uadilifu baina ya pande mbili. Jambo hili linawakera mno waislam na hasa ukizingatiya kuwa ipo njia mbadala nayo ni bima ya Kiislam (Takaful).

Harakati za kuomba kuwepo bima hii nchini zimeanza kitambo. Tangu mwaka wa 2012, mamlaka ya Bima (TIRA) ilifanya utafiti juu ya uwepo wa haja ya bima hii na utafiti huo ulionesha kuwa bima ya Kiislamu inahitajika nchini. Miaka iliyofuata mamlaka iliandaa taratibu za kutoa leseni na usimamizi wa bima aina hii (Takaful regulations) ambazo zilijadiliwa kwa kina na wadau na wataaalamu mbalimbali nchini hadi kuhitimishwa kwa ajili ya kusainiwa na kupelekwa Wizara ya Fedha. Mwaka 2018, katika mkutano wa kila mwaka wa Bima nchini uliofanyika Tanga, Waziri wa Fedha Mh. Mpango alikiri kuwa taratibu za bima hii zimechukuwa muda mrefu kukamilika na kuwa Waziri ataingilia kati (ministerial interventions) ili ziweze kusainiwa na kutumika.

Mwaka na miezi sasa tangu kauli hiyo itolewe, hatuna taratibu hizo na ilhali zipo kampuni ambazo zipo tayari jana kabla ya leo kuwekeza katika uendeshaji na utoaji wa bima hii nchini. Fursa za ajira zinapoteya na Mali za waislamu zinakosa bima ya Kiislamu mpaka kuangamiya kwa moto bila fidia kutokana na Waziri kushindwa au kulegalega katika kuidhinishwa kwa taratibu za bima hii. Hatutaki kuamini kuwa Waziri anashawishiwa na makampuni shindani yanayoona yatakosa biashara iwapo bima hii itaruhusiwa. Pia hatutaki kuamini kuwa Waziri hatambui haja na hamu kubwa ya Waislam na wananchi wote kuwa na bima yenye kusimama katika uadilifu.

Hivyo, tunamkumbusha kwa unyenyekevu mkubwa Waziri na wafanya maamuzi katika Wizara ya fedha, kuharakisha kupitishwa kwa taratibu hizo ili tuweze kupata wawekezaji zaidi katika huduma za bima nchini, kutengeza ajira, kuongeza matumizi ya bima kwa wananchi, kueleta ushindani na muhimu zaidi kuwawezesha waislamu kutumiya bima ambayo itawaezesha kupata fidia ya hasara za maafa ya moto na mengineyo.



No comments:

Post a Comment