Pages

Tuesday, July 14, 2020

UCHUMI WA KATI NA JAMBO LILILO MUHIMU ZAIDI


Siku chache zilizopita nchi yetu ilitangazwa kuwa sasa ni nchi yenye uchumi wa kati (middle income country). Wanasiasa wanaongoza serikali walitumiya fursa hiyo kudhihirisha furaha yao kwa kuona juhudi za muda mrefu zimezaa matunda. Wachumi wanaona hatuwa hii inafaida zake na hasara au changamoto zake. Na hili ni jambo la kawaida, iwe furaha kwa wanasiasa au iwe uchambuzi wa pande mbili -faida na hasara- kwa upande wa wachumi

Makala haya hayalengi kuwa upande wa wanasiasa wala wachumi wenye kupima maendeleo katika mizani ya pato la taifa. Makala haya inataka kubainisha kuwa pamoja na lengo hili la kuwa uchumi wa kati kufikiwa, tusisahau yaliyo muhimu zaidi na ambayo wenzetu waliondeleya (developed countries) wanalenga kulifikiya badala ya kuongezeka pato la taifa tu. Hii haimaanishi kuwa ongezeko la pato la taifa sio muhimu, la hasha. Lakini tufahamu kuwa ustawi wa nchi na watu wake haupo katika kuongeza kipato peke yake. Iwe kipato halisi au kama washindani waliokuwa nje ya serikali wanavyoona kuwa ni kipato cha katika makaratasi!

Wachumi wa Kiislamu kwa miaka mingi wamefikiria na kulenga katika kuelekeza sera za nchi katika kukuza kipato cha mwananchi kwa upande mmoja na kuhakikisha kuwa wananchi wanafuraha (Happiness). Hili la kipato linalenga kuhakikisha wananchi wanaondoka katika mtihani wa ufukara jambo ambalo
Mtume s.a.w alikuwa akimuomba Mola wetu amuepushe na ufukara. Na suala la kuwafanya watu wawe na furaha ni katika mafunzo ya Mtume s.a.w pale aliposema; amali au kitendo kizuri ni kufanya jambo kwa ndugu yako akafurahi au kuingiza furaha kwa ndugu yako!

Katika miaka ya 2010, wanasiasa na wachumi wa nchi zilizoendeleya wamezinduka kuona kuwa kile ambacho kwa miaka mingi wamekishughulikiya nacho ni kuongeza kipato cha watu wao,kuwa matajiri zaidi wakitarajiya kuwa kwa utajiri huo matatizo yote yatakwisha lakini la kustaajabisha ni kuwa pamoja na kuongezeka kipato katika nchi ya Amerika na Ulaya, lakini tafiti zinaonesha furaha haikuongezeka! Profesa Richard Layard na wenzake katika kitabu chao "The Origins of Happiness (2019)", wanauliza swali hili "jambo gani muhimu zaidi kwa mwanandamu (what matters most?) na kujenga hoja kadhaa kuwa fedha zilionekana kuwa ni muhimu mpaka hivi karibuni watu wakiipa fedha nafasi ya heshima. Lakini sasa hivi watu wengi duniani wameona na wanataka kutazamwa upya dhana ya maendeleo. Watu hawa wanakataa kuwa utajiri na kipato kuwa sera za maendeleo ya nchi na mtu binafsi yasiweke mbele zaidi kipato kikubwa kama ishara ya maendeleo na badala yake maendeleo yapimwe kwa kutazama watu wangapi wana furaha na maisha yao. Hivyo watunga sera wanapaswa kuzielekeza sera zao katika kuweka mazingira ambayo watu watakuwa na ustawi na furaha.

Kwa kulitambuwa jambo hili na umuhimu wake, nchi ambazo ni sehemu ya OECD wameazimiya kuwa sera za nchi zao zijielekeze katika ustawi na watu wao wawe na furaha. Hivi sasa kuna nchi kadhaa ambazo zimefikiya kuwa na mawaziri wa kuhakikisha watu wanaishi kwa furaha (Ministers for Happiness) kama vile UAE na sehemu nyingine. Umoja wa Mataifa umeifanya Machi 20 kila mwaka ni siku ya kimataifa ya furaha (International Day of Happiness).

Kadhalika tafiti na ripoti zimekuwa zikifanywa na kuchapwa kila mwaka ili kupima kiwango cha furaha cha wananchi wa nchi mbalimbali duniani. Kwa mfano ripoti ya mwanzo ilichapwa mwaka 2012 na ripoti ya mwaka huu -World Happiness Report 2020, inaonesha kuwa Tanzania ipo chini katika kuwa na watu wenye furaha! Bila shaka, ripoti hizo zinaweza kubishaniwa na hoja kutolewa za kuunga mkono au kuzipinga ripoti hizo. Ikiwa tutaziunga mkono au kinyume chake, jambo moja tunapaswa kukubaliana kama watanzania katika kuendeleza uchumi wa watu wetu nalo ni tusisahau yale ambayo yanawapa ustawi na furaha wananchi wetu! Jambo hili hatuna budi kulitazama kwa kina na kulipima wenyewe kila mwaka au baada ya miaka ili tuhakikishe kuwa kukuwa kwa kipato kunaenda sambamba na kuongezeka furaha na sio karaha au kuongezeka matatizo ya akili au watu kujitowa uhai bila sababu kama ilivyo leo katika nchi nyingi zilizoendeleya.

Katika kufikiya azma hii, Mtume s.a.w anatukumbusha na kutufunza aliposema "Katika mambo yenye kumpatiya mtu furaha ni kuwa na jirani mwema, kuwa na chombo kizuri cha usafiri na kuwa na makazi yenye nafasi."Wale ambao wamejaaliwa mambo hayo matatu basi wakithirishe kushukuru, na wale ambao wamekosa hayo, ni wajibu wa watunga sera kuweka mazingira mazuri ili vitu hivi avipate kila mwananchi wa Tanzania pamoja na kuwa na elimu bora na huduma bora za afya, maji safi, umeme wa uhakika, haki za binadamu zenye kuheshimiwa n.k. Tuanzie katika familiya zetu, mitaani, kata, vitongoji, vijijini, wilayani, mkoani na taifa lote kwa ujumla. Sote twenye dhima ya uongozi katika maeneo hayo, tutekeleze wajibu wetu wa kuweka mazingira mazuri ya ustawi na furaha!

No comments:

Post a Comment