Pages

Wednesday, July 29, 2020

MAENDELEO TUYATAKAYO


Tupo katika mwaka wa uchaguzi mkuu wa nchi nzima. Vyama mbalimbali vitarudi kwa wananchi kunadi sera zao na mipango yao ya kuwaleteya wananchi maendeleo. Je ni maendeleo gani tuyatakayo watanzania na waislamu?

Dhana ya Maendeleo.

Neno hili "Maendeleo" (Development), hupendwa sana kutumiwa na wanasiasa wanapojinadi kwa wananchi. Wataalamu wa lugha ya Kiingereza wanasema kuwa neno hili "development" lilianza kutumika katika kuelezeya hatua za ukuaji wa viumbe katika miaka ya 1756. Na limekuja kutumiwa na wachumi katika miaka ya 1902 na kuendeleya likimaanisha kuwa ni hali ya kupiga hatuwa za kiuchumi (state of economic advancement). Dhana hii ya maendeleo ya kiuchumi ilishika kasi zaidi baada ya vita vya pili vya dunia na mijadala kadhaa ikifanyika mpaka kuja kuibuka kwa somo maalum liitwao "development economics." ambalo hufunzwa katika vyuo vikuu mbali mbali ulimwenguni.

Kimsingi kuna tafsiri nyingi sana kutoka kwa wachumi kuhusiana na swali hili, "maendeleo" ni kitu gani? Wengi wetu neno maendeleo tunalihusisha tu na weingi wa fedha, hali nzuri ya maisha inayomwezesha mtu kuweza kujikimu bila hofu, kuwa na miundombinu imara kama vile barabara, maji, shule, umeme, vituo vya afya, kukuza uchumi ili kutowa ajira nyingi nakadhalika. Mara nyingi viongozi na wanasiasa hukusudiya maana hii wanaposimama kujinadi majukwaani kuomba kura. Haya ni sehemu moja tu ya maendeleo.

Maendeleo katika Uislam.

Wachumi wa Kiislamu wamefanya kazi kubwa katika kubainisha mtazamo wa Uislamu kuhusu maendeleo. Pamoja na kuwepo mitazamo mbalimbali, wanachuoni hawa wanaona kuwa maendelo ni lazima yajumuishe na yahusishe maeneo matatu muhimu na makubwa. La kwanza, uwepo wa fursa kwa wote na uhuru wa mtu binafsi kujiendeleza mwenyewe bila hofu wala upendeleo (individual human self-development without fear or favour).Pili, uwepo wa mazingira rafiki na bora yenye kumwezesha mtu kufikiya malengo yake kipindi chote (physical and material development of the earth). Na la tatu, kuwepo kwa haya mawili kwa watu wote katika jamii husika (development of society as whole). Uislam unaona kuwa eneo la kwanza ni muhimu zaidi na ndio chachu ya kupatikana maendeleo katika maeneo haya mengine. Anasema Mchumi mmoa wa Kiislam Profesa Abdul Hamid Abdul Aziz "Mazingira ya mwanadamu yaandaliwe kutowa fursa na uhuru wa kubadilika kutoka hatuwa moja kwenda hatuwa iliyobora zaidi sio kimali tu na bali na kiimani na muruwa mwema (material and spiritual development)."

Uislam unaona maendeleo yoyote yale lazima yamwezeshe Mtu ambaye ni Khalifa wa Mwenyezi Mungu, aweze kutoka katika umasikini wa kipato, fikra, imani na utamaduni na kueleya katika mabadiliko ambayo yatamwezesha kuwa na utajiri wa maarifa, wingi wa Imani kwa Muumba wake, muruwa mwema au tabia njema, fikra madhubuti za kielimu na kuyamudu mazingira yake muda wote. Mtu huyu awe anajitambuwa mwenyewe, anatambuwa lengo la kuumbwa kwake, anamtambuwa Muumba wake, na majukumu aliyopewa kama Khalifa wa Mwenyezi Mungu ambayo yanalengo la kumtowa katika upotofu na giza na kumwingiza katika nuru na uongofu. Kwa lugha ya Qur'an hawa ndio Ar Rashidun (walioongoka na walioendeleya)

Maendeleo katika sura hii ndio ambayo Quran inayaona kuwa ni fadhila na neema kubwa pale Mola aliposema "Lakini Mwenyezi Mungu amekupendezeeni Imani, na akaipamba katika nyoyo zenu, na amekufanyeni muuchukie ukafiri, na upotovu, na uasi. Hao ndio walio ongoka (walioendeleya).Kwa fadhila za Mwenyezi Mungu na neema zake. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua, Mwenye hikima (49:7-8). Mtume salallahu alayhi wasallam amesema " Amefaulu (katika kila jambo) yule ambaye ni Muislam wa kweli aliyejisalimisha katika uongofu wa Mola wake, akaruzukiwa rizki yenye kumtosheleza mahitaji yake katika maisha ya Ulimwengu na Moyo wake ukawa wenye kushukuru na kukinai (usiokuwa na pupa na vitu au anasa za kilimwengu)." Vile Mtume s.a.w amesema " Sifa nne mwenye kuwa nazo, basi asiwe na hofu juu ya lolote alilolikosa ulimwenguni. Ya kwanza, Uaminifu (trustworthy) (dhana pana sana yenye kujumuisha kuwa Mwaminifu juu ya amri za Mola wako na juu ya yale uliyoaminiwa na viumbe wenzio iwe siri, kazi, au mali n.k). Ya pili, Ukweli (truthful) katika kauli zako na matendo yako ya kila siku, humdanganyi mtu wala huthubutu kumdanganya Muumba wako. Ya tatu, kuwa na tabiya njema zenye kupendeza hata watu wakawa hawaudhiki kwa kuwepo kwako pamoja nao, ikawa mfano wako ni sawa na mtende wenye kutowa mazuri zaidi kuliko unayochukuwa kutoka katika ardhi na kwa watu na ya mwisho, mwenye kutosheka na chakula chako cha kila siku." [Imepokewa na Imam Ahmad katika Musnad Ahmad].

Pamoja na hayo, Uislam umempa jukumu mwanadamu aindeleze ardhi au ulimwengu na mazingira yanayomzunguka kwa kumtaka awe Mus-liheeena (mwenye kufanya wema) na sio Mufsideena (mwenye kuharibu). Mola anasema "Na utafute, kwa aliyo kupa Mwenyezi Mungu, makaazi ya Akhera. Wala usisahau fungu lako la dunia. Nawe fanya wema kama Mwenyezi Mungu alivyo kufanyia wema wewe. Wala usitafute kufanya ufisadi katika ardhi. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi mafisadi." (28:77).

Maendeleo Tuyatakayo.

Kwa kuzingatiya kuwa dhana ya maendeleo ni mada pana mno Kiuchumi na katika Uislam na ambayo makala haya haitoshi kuijadili kwa urefu wake bali kukumbusha tu Waislam na wasomaji wafahamu Uislam una mtazamo wake na mafundisho yake yanalenga kumleteya maendeleo mwanadamu katika maeneo yake yote muhimu; kiimani, kiakili, kitabiya, kimali, kiafya na kimaisha kwa ujumla wake na sio kama nadharia za kimagharibi ambazo zimechukuwa baadhi ya mambo haya na kuyaacha mengine. Hivyo maendeleo tuyakayo ni lazima yajikite katika ujumuifu mambo haya yote na katika kuelezea nukta hii nitatowa mifano miwili tu.

Maendeleo ya Kiimani.

Mwanadamu anahitajio la kuamini katika maisha yake. Kwa kuwa hili halimwepuki, anaweza kuishiya kuamini ipasavyo au kupoteya katika imani yake hiyo. Na haiwezekani bali ni ujuha uliofurutu ada kuwa mwanadamu anaweza kudai yeye hana anachoamini. Hivyo binadamu anahitaji maendeleo ya kiroho na kiimani (spiritual development). Je kama taifa tunamjengeya imani gani mwananchi wa Tanzania? Ukitazama vyama mbalimbali, utaona kuwa vyama hivyo vina ambayo vinayaamini kwa mfano kipo chama kinachoamini kuwa "Binadamu wote ni Sawa, Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.Ujamaa na kujitegemea ndiyo njia pekee ya kujenga jamii ya watu walio sawa na huru." Kwa hiyo, vyama vina imani zake mbalimbali.

Je ni maendeleo gani ya kiimani tuyatakayo? Kama Waislamu, maendeleo ya kiimani tuyakayo ni kuwa na taifa linaloamini uwepo wa Mwenyezi Mungu Mmoja na sifa zake tukufu na kadhalika. Hivyo kwa kuzingatia imani hii, wale wanaodai kutaka kutuleteya maendeleo hawatopuuza mchango wa wale ambao wanatukumbusha uwepo wa Mwenyezi Mungu na muongozo wake kama ambayo hali ilivyo sasa hivi. Kwa mfano, kwa nini hamna walimu walioajiriwa kufundisha somo la dini mashuleni kama ilivyo masomo mengine? Je kwa nini serikali haitowi msaada katika kuchapa na kusambaza vitabu vya elimu ya dini mashuleni? Majibu mepesi tunayoweza kuyapata ni kuwa serikali haijihusishi na mambo ya dini au serikali haina dini. Ikiwa kuyafanya haya ni kujihusisha na mambo ya dini kana kwamba dini ni jambo baya kabisa basi ni wazi kuwa eneo hili la kimaendeleo limewachwa makusudi. Sisi tunaona kuwa serikali kama ambavyo inasimamia taasisi zote za dini bili kuziingiliya uendeshaji wake hivyo hivyo inayo nafasi ya kutowa machango wake katika eneo hili muhimu na nyeti la kimaendeleo. Hivyo, iwapo wanasiasa wetu wanadai na kuamini Mungu yupo, hatuna budi kuendeleza imani hiyo kwa kiwango cha kuthamini walimu wa masomo ya dini katika nchi yetu.

Maendeleo ya Kitabia

Mwanadamu anatabia zake za kimaumbile na zile anazojifunza kila siku na kuamuwa za kuchukuwa na kuziacha. Maendeleo yenye kubadilisha tabiya mbovu kuelekeya katika tabia nzuri (moral development) ni kipaumbele kinachostahiki . Je kama taifa tunafunza, kusimamiya na kuhimiza tabiya gani kwa wananchi wetu bila kujali mwanachama wa chama au la? Nchi yetu imeshuhudiya na inaendeleya kushuhudiya mmomonyoko wa maadili mema kwa vijana na wazee wetu. Haya ni matokeo ya kutofunza na kusimamia maadili ipasavyo katika ngazo zote. Watu wafunzwe tabia ya ukweli, uaminifu, uchapakazi, kufanya mambo kwa ajili Mungu n.k. Kama taifa tumewaachia watu fulani kufunza maadili kama vile viongozi wa dini, wazazi au mtu binafsi. Je inatosha? Jawabu ni haitoshi. Kama ambavyo tunafunza masomo ya uraia (civic education), mazoezi (physical education) n.k tunahitaji uwekezaji katika kufunza maadili mema kama taifa na kuyasimamia. Haitoshi kuwa na watu ambao wanasema "Nitasema kweli daima, fitina kwangu mwiko" na kisha wanapoenda kinyume chake kwa kusema uongo hadharani na kuleta fitina ikawa taifa halichukuwi hatuwa zozote. Wamesema wanchuoni wa tabia kuwa "Taifa / Umma wowote ule kuwepo kwake na kubaki kwake kunategemeya uwepo wa maadili yake. Iwapo maadili yake yataondoka, basi na umma huo utakuwa umeondoka hata kama vizazi vingalipo."

Hivyo maendeleo tuyatakayo yawe jumuishi kwa watu wote, yenye mtazamo mpana na mtambuka ambayo yatajikita kumbadilisha mwanadamu mwenyewe kuwa kiumbe bora kama Mungu anavyotaka awe na kuimarisha mazingira yake na kustawisha jamii yote kwa ujumla. Maendeleo ambayo yanatowa fursa kwa wote kujiendeleza kwa uhuru bila uonevu wala kupendelewa au kukandamizwa. Maendeleo ambayo utu wetu unaheshimiwa, unalindwa, unaimarishwa na kuendelezwa na sio kudunishwa, kupuuzwa au kudumazwa.


No comments:

Post a Comment