Pages

Tuesday, July 7, 2020

UCHUMI WA KIISLAM NA UCHUMI WA KIBEPARI


Ulimwengu umeshuhudia aina kuu mbili za mifumo ya uchumi. Mifumo ya uchumi ya wanadamu na mfumo wa uchumi wa Mwenyezi Mungu. Watu walipojieka mbali na muongozo wa dini zao, waliunda dini mpya na mifumo mipya ya kuendesha maisha yao kwa kutarajiya kupata maendeleo au furaha au ustawi wa jamii zao. Je wameyapata maendeleo, furaha na ustawi wa jamii zao? Na je maendeleo au furaha au ustawi huo unaishia maisha ya dunia pekee au na maisha baada ya kifo? Yoyote yule anayejishughulisha na uchumi binafsi, wa jamii au wa nchi, yampasa ajiulize iwapo njia au mikakati anayofuata itampa utulivu duniani na malipo akhera. Hili ni suali muhimu ambalo yataka turudi katika kulinganisha baina ya mfumo wa uchumi wa Kiislamu na mfumo ya wanadamu kwa mfano ubepari (capitalism).

1. Itikadi.

Mfumo wa uchumi wa Kiislamu umejengwa na kusimama katika kuamini uwepo wa Muumba wa ulimwengu na walimwengu, Mwenye kuruzuku neema mbalimbali ni Mola mmoja asiyekuwa na mshirika. Ameumba ulimwengu kwa ajili ya matumizi ya mwanadamu na shughuli zake za kiuchumi hazina budi kutambuwa mchango wa Mola katika natija anayoipata. Je umeona moto ambao mnautumia? Je ni nyinyi ambao mlioanzisha au ni yeye? Je mmeona maji mnayokunywa? Ni nyinyi mlioyateremsha katika hazina zake au ni yeye? Je mmeona mbegu mnazozipanda ardhini? Je ni nyinyi mnaootesha mazao mbalimbali kwa mbegu hizo au ni yeye? (Surat Waqiah). Kiitikadi, mfumo huu unatambuwa kuwa yupo ambaye bila yeye hamna linalowezekana kwa juhudi ya mwanadamu peke yake. Hii haimaanishi kuwa mtu asijishughulishe, hapana afanye harakati mbalimbali za kujileteya maendeleo huku akijuwa kuwa hizo ni sababu tu na yeye Mola ndio anayesababisha sababu hizo zilete matokeo fulani. Hivyo, kwa kwa itikadi hii, yeyote anayejishughulisha katika kukuza uchumi wake na wa watu wake, hana budi vilevile kutambuwa mipaka iliyowekwa na yule ambaye ulimwengu ni milki yake. Kuna shughuli ambazo amezihalalisha na nyingine ameziharamisha. Hivyo uchumi wa Kiislam, unaona rasilimali zilizopo ni fadhila za Mola kwa wanadamu, zinatakiwa kutumika kwa njia ya halali, kuimarisha ustawi wa mtu na jamii yake na matokeo ya matumizi hayo daima yaambatane na shukrani kwa Muumba.

Mifumo ya uchumi wa kibinadamu inasimama katika kuamini kuwa ulimwengu umejitokeza tu bila kuumbwa na Mola. Nadharia mbalimbali za kuibuka kwa ulimwengu zimearifu kuwa Ulimwengu ulitokeya tu. Rasilimali hizi ni chache na hivyo hamna budi kufanya juhudi ya kila namna ili kuweza kuzimiliki rasilimali hizo kwa maslahi binafsi(ubepari) au maslahi ya jamii yote (ujamaa). Mfumo wa kibepari umeyaweka maendeleo na furaha na ustawi katika matashi na juhudi za mtu mwenyewe. Ni wewe mwenyewe unayeweza kujiendeleza au kujididimiza. Ukitumia rasilimali vizuri utapata natija nzuri au ukitumia rasilimali vibaya utapata matokeo mabaya, suala la uzuri na ubaya ni kwa mizani ya mwanadamu mwenyewe. Apataye ni mwerevu na aliyekosa ni mlegevu! Hamna la halali au haramu isipokuwa lile ambalo sheria za nchi imebainisha kuwa ni halali au haramu hata kama sheria hiyo inaenda kinyume na Sheria ya Mwenyezi Mungu. Hivyo, rasilimali zilizopo ni chache, ni zawadi ya asili, anayezimiliki ni mwerevu na kuzitumia rasilimali hizo ni kwa matashi binafsi ya kujipatiya furaha na ustawi kwa mtu binafsi bila kujali ustawi wa jamii nzima.

2. Uzalishaji Mali.

Mfumo wa uchumi wa Kiislamu unahimiza katika kuzalisha mali. Mali hiyo ni kila kitu chenye manufaa kwa watu katika maisha yao. Mali hiyo iwe ni zao la kazi ya halali na sio wizi au kwa hila mbalimbali. Mali inazalishwa kwa kulima, kuvua, kuzalisha, kutengeneza, kununuwa na kuuza n.k. Binadamu katika kuzalisha mali hana budi kuchunga asizalishe mali kwa njia za haramu au asizalishe mali haramu.

Mfumo wa kibepari pia unahimiza kuzalisha mali mbalimbali ili kupata utajiri ambao utatumiwa kwa maslahi ya mwenye mali mwenyewe. Mali hiyo ni kitu chochote kinachoweza kumilikiwa. Uzalishaji ni jambo huru kwa mtu kuamuwa mwenyewe anataka kuzalisha nini. Haidhuru kitu hicho kiwe ni kwa manufaa au chenye madhara kwa watu kwa mfano wa sigara, dawa za kulevya, ulevi, mirungi, filamu za ufuska, biashara ya bidhaa feki nakadhalika. Uhuru wa mtu ni kitu kitakatifu katika ubepari kiasi ambacho dola inawajibu wa kuulinda uhuru huo hata kama unamleteya madhara huyo mwenye kupewa uhuru huo. Hivi karibuni, huko amerika imekuwa halali kulima na kuvuta bangi katika baadhi ya majimbo ya nchi hiyo. Baada ya uzalishaji sigara, pombe na picha za ufuska, sasa bangi pia ni rukhsa na pengine wakaruhusu dawa za kulevya siku za usoni.

3. Matumizi ya Mali.

Mfumo wa Uchumi wa Kiislamu unahimiza matumizi ya wastani ya mali na matumizi yenye kujali wengine. Mali uliyonayo ni amana kwa matumizi yako ya msingi na pia kuwatazama wengine. Uislam unakataza matumizi ya anasa na israfu na uharibifu wa mali. Kama ilivyokuwa katika kuchuma kwa kufuata amri za Mungu, na katika kuitumia pia ni lazima kufuta maelekezo ya Mungu. Mungu ameelekeza kuwa mali itumiwe kwa wastani kwa ustawi wa mwenye mali na familia yake, na jirani zake na jamii yake.

Mfumo wa kibepari unaona suala la matumizi ni eneo la uhuru wa mtu lisilokuwa na mipaka. Kama alivyotafuta kwa nguvu zake na matumizi ni kwa matashi yake. Hamna kizuizi katika matumizi isipokuwa sheria za nchi ambazo hata hivyo baadhi yake zinaonekana kuwa ni kandamizi dhidi ya uhuru wa binadamu. Mfumo huu kwa uhalisia unahimiza matumizi ya anasa na israfu na kununuwa vitu mara kwa mara (consumerism) kama njia ya kuthibitishia wengine kuwa wewe ni mwenye uwezo wa kumudu chochote ukitakacho. Mfumo huu unahimiza mashindano ya vitu badala ya utu. Wajibu wa mtumiaji mali unaishia katika kujistawisha na kujifurahisha yeye mwenyewe hata kama umezungukwa na majirani wanaolala na njaa au wanauguwa maradhi mbalimbali kwa kushindwa kumudu gharama za matibabau au kuishi katika ujinga kwa kushindwa kumudu gharama za elimu.

4. Usambazaji wa Mali.

Mfumo wa uchumi wa Kiislamu umeweka njia mbalimbali za kuigawa mali miongoni mwa wanajamii ili wote wawe na ustawi unaohifadhi heshima ya binadamu kama kiumbe bora ulimwenguni. Njia ya Zakat ni moja wapo. Kila mwenye mali analazimika kila mwaka kugawa sehemu ndogo ya mali yake kwa ajili ya wale ambao hawana kitu ili na wao waweze kufurahi na kustawi katika jamii yao. Mali inapaswa kuzunguka na sio kuhodhiwa na wachache! Njia nyingine ni sadaka na waqfu ambazo zinapelekeya mali kugawiwa kwa watu mbalimbai katika jamii ili kuinuwa hali zao.Serikali yenye kufuata mfumo huu, inajali raia wake kwa kuhakikisha wale ambao hawana uwezo wa kujikimu wanasaidiwa na serikali kupata mahitaji ya msingi yenye kuhifadhi utu wao na heshima yao.

Imesemwa kuwa Ubepari hauna roho. Kila kinachopatikana baada ya kutowa kodi stahiki (na mara nyingi kodi hiyo huepukwa kwa udanganyifu), mwenye mali hana wajibu wa kumsaidiya yoyote. Yoyote mwenye shida arudi kwa serikali yake, kwa msaada. Sio wajibu wa mfanyabiashara au mwenye mali kuhakikisha mali hiyo inawasaidia wengine katika jamii yake na hata kwa familia yake. Mzazi katika mfumo wa kibepari hana wajibu hata wa kumsaidia mwanawe aliyebaleghe kwa kumpa mtaji wa bure, mtoto katika umri huo ni wa serikali kumtazama na kujitafutia mwenyewe. Ni mimi mimi! (Man eat man society). Hakuna cha bure katika ubepari. Imesemwa ukipewa cha bure ujuwe wewe ndio bidhaa yenyewe ambayo inauzwa kwa wengine! Tunayaona haya katika mitandao ya kijamii. Ni bure kujiunga lakini kumbe taarifa zetu za kimtandao zinauzwa kwa pesa nyingi kwa wengine!


5. Fedha (Capital).

Mfumo wa uchumi wa Kiislam unaona kuwa fedha au mtaji unanafasi yake lakini sio mama wala msingi mkuu wa uzalishaji. Bali binadamu, mwenye nguvu kazi na maarifa akisuhubiana na mtaji unaohitajika hupelekeya katika uzalishaji na hivyo viwili hivyo havitengani katika uzalishaji. Fedha inahitajika kujumuika na binadamu mwenye maarifa na ujuzi katika uzalishaji wenye tija. Hivyo, vyote viwili vinatakiwa kuthaminiwa kwa uadilifu na bila kimoja kumuelemeya mwenzake kuwa ni eti ni bora zaidi. Hivyo ni marufuku katika uchumi wa Kiislam, mwenye fedha kutowa fedha kwa mkopo na kudai nyongeza bila kuwa tayari kubeba hasara inayotakana na shughuli inayofanyika na fedha hizo.

Ubepari (Capitalism) unaona kuwa fedha na mtaji ndio mama na msingi mkuu wa uzalishaji. Hivyo fedha pekee inaweza kuzalisha fedha nyingi zaidi kwa kokopeshwa kwa riba mara dufu na kumpatiya mwenye mtaji huo fedha zaidi bila kujali mchango wa binadamu katika kuzalisha. Watu ni watumishi wa mtaji na hivyo mtaji unastahiki kupata faida zaidi kuliko binadamu anayeufanya mtaji huo uzalishe zaidi. Kwa fikra hizi, ulimwengu leo unashuhudia mpasuko mkubwa sana baina ya matajiri na masikini. Kwa kuwa matajiri hao wanatumia mitaji yao katika kujipatiya faida kubwa kwa mfano wa riba hali ya kuwa wao wenyewe hawafanyi kazi yoyote. Mfumo huu hauzingatii uadilifu baina ya wenye mitaji na wenye kufanya kazi! Si ajabu Bilionea Ray Dalio, amesema kuwa "Capitalism is failing us (Ubepari unatufelisha katika maisha)."

Hitimisho.

Pamoja na kuwa uchumi wa Kiislamu ulishamiri katika wakati wa Mtume s.a.w na makhalifa zake waongofu na athari zake zikiwepo katika dola zilizokuwepo chini ya himaya ya Ukhalifa, leo ni nchi chache ambazo zina mwelekeo wa kushikamana na uchumi wa Kiislam. Habri nzuri ni kuwa mfumo wa uchumi wa Kiislam umekuwa ukifanyiwa utafiti kwa muda sasa ili uweze kufuatwa katika zama hizi baada ya kuwa ulipigwa vita baada ya kuanguka dola za Kiislam na kuingia ukoloni wa nchi za magharibi ambao ulifanya juhudi ili kufuta athari ya uchumi huu.

La kusukitisha zaidi ni kuwa binadamu katika zama hizi, wengi wetu tumekuwa mabepari na mifumo ya uchumi wetu imekuwa ikielekeya katika mfumo huo zaidi kuliko mifumo mingine. Hata hivyo, zipo tofauti katika mfumo huu wenyewe, kuna ubepari wa dola (State / political capitalism) ukiongozwa na China na ule wa nchi za kimagharibi (Liberal capitalism). Mwandishi wa Capitalism Alone, bwana Branko ameeeleza kwa undani kushamiri kwa aina hizi za ubepari na dosari zake akisisitiza kuwa mabadiliko lazima yafanyike haswa katika ubepari wa nchi za magharibi. Katika maependekezo yake, ameshauri dola zifanye yafuatayo:
1. Kuhamisha mitaji na umiliki wa mitaji hiyo kwa kuwapa nafuu ya kodi watu wenye vipato vya kati na kuwatoza kodi kubwa kabisa matajiri na kuweka kodi katika mali za mirathi. (deconcentrating capital and wealth ownership through tax advantages that give the middle class a bigger stake in financial capital and a corresponding increase in the taxation of the rich, coupled with higher taxes on inheritance).
2. Serikali zifanye uwekezaji mkubwa katika kuboresha elimu na kutowa fursa sawa kwa wazalishaji na wawekezaji. Hii inajumuisha serikali kufanya biashara na wawekezaji wa kati kwa kuwapatia tenda mbalimbali. (He also calls for a significant boost in public investment to broaden access to high-quality education and enhance equality of opportunity.)
3. Serikali kuweka kikomo cha michango ya matajiri kwa wanasiasa au vyama vyao na watunga sera mbalimbali ili matajiri hao wasihodhi mfumo wa kisiasa na kujinufaisha zaidi kupitiya wanasiasa ambao watakuwa wanawafungulia njia zaidi za kumiliki mitaji na kuwekeza pasi na ushindani ulio wa haki. (Strictly limited and exclusively public funding of political campaigns to reduce the ability of the rich to control the political process is another necessary reform).

Hizi ni hatuwa za mwanzo na mengi zaidi yanapaswa kufanywa ili kuiepusha nchi kama Tanzania, isije kujikwaa katika dosari za ubepari wa kimagharibi.


No comments:

Post a Comment